Mahitaji ya Udongo na Mbolea katika kilimo cha Mahindi


Mahitaji ya udongo na mbolea katika kilimo cha mahindi

Habari, na karibu tena katika muendelezo wa mafunzo yetu ya kilimo cha kisasa. Leo tutaangazia kwenye mahitaji ya Udongo na  Mbolea katika kilimo cha Mahindi.
Karibu …
Mahitaji ya udongo na mbolea ni muhimu kwa ajili ya ukuaji wa mmea wowote ule, hata hivo mahitaji hayo hutofautiana kati ya mmea moja na lingine kutokana na kutofautiana kwa sehemu ya zao (product) katika hiyo mimea (yaani economic part of a plant). Kwa mfano: mahindi, mpunga sehemu ya zao ni mbegu/punje, wakati nyanya, na bilinganya zao lake ni tunda nakadhalika viazi zao lake ni mizizi!
Hivyo basi mahitaji ya udongo na mbolea katika kilimo cha mahindi ni tofauti na mazao mengine, endelea....



UDONGO
Udongo una rutuba ya asili yaani virutubisho katika udongo, mboji (organic matter), na viumbe mbalimbali vinavyoishi kwenye udongo. Rutuba ya udongo inategemea sana hali ya udongo kikemia, kibiolojia na kifizikia.

Makundi Ya Udongo
Kuna makundi makuu matatu ya udongo, kutokana na ukubwa wa chengachenga za udongo:
Kichanga (Sand soil) - una uwezo mdogo wa kuhifadhi maji na unyevunyevu. Hivyo, hukauka upesi.
Tifutifu (Loam soil) - unahifadhi maji vizuri na upatikanaji wa maji na virutubisho kwa mimea ni mkubwa.
Mfinyanzi (Clay soil) - unahifahdi maji mengi zaidi, bali upatikanaji wa maji na virutubisho kwa mimea ni mdogo.

Vipimo vinavyoonyesha hali ya rotuba ya udongo ni:
• Tindikali ya udongo
• Kiasi cha mboji
• Kiasi cha Naitrojeni, Fosfati, Potashi, Salfa, Chokaa (Calcium) na Magnesium. Vilevile kiasi cha zinki, shaba, manganese na boroni vinapimwa.

pH ya udongo (Soil pH)
pH ni kipimo kinachoonyesha kiwango cha tindikali au nyongo katika udongo. Udongo waweza kuwa tindikali (ph ndogo kuliko 7), nyongo (ph kubwa kuliko 7), au katikati (neutral) - ph ya 7. Tindikali au nyongo ya udongo hupimwa kwa kutumia pH mita. Mazao mengi hustawi zaidi katika udongo wenye hali ya tindikali ya wastani (kipimo cha pH 5.5 hadi 7.0).
Mahindi hustawi kwenye udongo wa tifutifu wenye tindikali ya wastani na virutubisho vya kutosha.


MBOLEA
Mbolea ni chakula cha mimea, ambayo ni mchanganyiko wa virutubisho mbalimbali vinavyoongezwa kwenye udongo au vinavyowekwa moja kwa moja kwenye mimea ili kuongeza ukuaji na uzalishaji wa mimea.
Virutubisho hivyo ni pamoja na madini muhimu kama vile naitrojeni, fosfati na potashi. Madini mengine ni pamoja na salfa, chokaa (calcium), magnesium, boroni, shaba, chuma, manganese, molybedenum na zinki. Haya madini kwa asili, yanapatikana katika udongo kwa viwango tofauti. Yanapopungua kutokana na kilimo, inabidi yaongezwe kwa kutia mbolea.

Aina za mbolea
Kuna aina mbili kuu za mbolea ambazo ni:
1. Mbolea za asili (organic fertilizers)
    2. Mbolea za viwandani (inorganic or industrial fertilizers)

Mbolea Za Asili (Organic Fertilizers)
Hizi ni mbolea zinazotokana na wanyama na mimea. Mbolea za asili ni kama vile: 
     i. Mbolea vunde: inajulikana pia kama biwi au compost. Hutokana na mchanganyiko wa manyasi au mabaki ya mbao na samadi na majivu.
      ii.  Samadi: kutoka kinyesi cha wanyama kama mifugo na ndege.
     iii.  Mbolea za kijani: hutokana na kupanda mimea aina ya mikunde ambayo hukatuliwa na kuchanganywa na udongo.
    iv.  Majivu: ni mbolea ya asili yenye madini aina ya potashi kwa wingi, fosfati, chokaa na magnesium.
      v.  Matandazo (mulch): ambayo baadaye yakioza huwa mbolea.

Mbolea Za Viwandani (Inorganic Fertilizers)
Hizi ni mbolea zinazotengenezwa viwandani kwa kutumia virutubisho mbalimbali kwa kufuata viwango maalum vilivyowekwa ili kukidhi mahitaji ya mimea. Mbolea hizi zinatengenezwa kwa lengo maalum la kupata aina na kiasi fulani cha kirutubisho/ virutubisho vinavyohitajika na mimea.

Mbolea Za Kupandia Mahindi
Mbolea maarufu za kupandia katika soko la Tanzania ni: TSP, DAP, Minjingu Phosphate na Minjingu Mazao. Lakini zile ambazo zimechaguliwa kwenye mradi wa ‘Kukuza matumizi ya Minjingu Phosphate’ ni DAP, Minjingu Phosphate na Minjingu Mazao.

                  1.            Diammonium Phosphate (DAP)
Ina virutubisho viwili - naitrojeni ambacho kiko kwa kiwango cha asilimia 18, na fosfati (P2O5) ambacho kiko kwa kiwango cha asilimia 46. Inapatikana katika hali ya chengachenga (granules).




                     2. Minjingu Phosphate
Ina kiwango cha fosfati (P2O5) asilimia 29 na inatumika zaidi kwa kutoa kirutubisho hiki. Lakini inaongeza vilevile kirutubisho cha chokaa (calcium) ambacho kipo kwa kiwango cha asilimia 40. Chokaa inasaidia vilevile kukabili tindikali (acidity) ya udongo.




                     3. Minjingu Mazao
Hii ni mbolea mpya inayotokana na Minjingu Phosphate lakini imeongezwa virutubisho vingine vitano ambavyo ni naitrojeni (10%), salfa (5%), zinki (0.5%), shaba (0.5%), boroni (0.1%), pamoja na chokaa (25% CaO) na magnesium (1.5% MgO). Virutubisho vilivyoongezwa hususani naitrojeni na salfa ni vile ambavyo vinakosekana katika aina nyingi za udongo.
Zinki, shaba na boroni vimeongezwa kwa tahadhari kwa sababu vinaonyesha dalili za upungufu katika baadhi ya maeneo. Minjingu Mazao iko katika hali ya chengachenga.



Jinsi ya kuchagua mbolea ya kupandia
Mbolea za kupandia hasa Minjingu Phosphate na Minjingu Mazao zinahitaji hali maalum ya udongo ili ziweze kufanya kazi vizuri.
Kwa mfano hali ya tindikali ya udongo inabidi iwe chini ya 6.2 ili mbolea za Minjingu ziyeyuke kwa kiwango cha kutosha. Kwa udongo wenye tindikali zaidi ya 6.2, tumia DAP wakati wa kupanda. Ikiwa kuna upungufu wa potashi, tumia mbolea zinazorejesha madini hayo.

Tumia mboji pamoja na mbolea za viwandani ili kuongeza mazao. Mboji huwa haibebwi na mvua na faida yake hudumu kwa muda mrefu. Mboji husaidia udongo kuhifadhi maji na virutubisho. Zinapowekwa kwenye mashimo ya kupandia mbegu ni vyema kufukia mbolea kabla ya kuweka mbegu (kutenganisha mbolea na mbegu).

Dalili Ya Upungufu Wa Virutubisho Mbalimbali
1. Upungufu Wa Naitrojeni (Nitrogen)
Kwa ujumla mmea unakuwa mdogo, mwembamba na hutoa suke dogo, na mwishowe hutoa mazao kidogo (picha A). Kama upungufu ni mkubwa sana mmea unaweza usitoe mhindi kabisa.

Kupungua kwa kasi ya ukuaji wa mmea - ambayo husababisha mmea kudumaa. Rangi ya kijani kwenye mmea hufifia na kugeuka taratibu kuelekea kwenye njano. Upungufu ukiwa mkubwa sana, majani hugeuka rangi ya njano kutoka pembeni. Majani yaliyokomaa ndio huanza kugeuka. Majani ya mwanzo hukauka mapema kwenye mimea yenye upungufu kuliko ile yenye naitrojeni ya kutosha.

 


2. Upungufu Wa Fosfati (Phosphorus)
Dalili ya kwanza ni kupungua kwa kasi ya kukua na mashina kuwa membamba.
Upungufu ukiwa mkubwa, mmea unakuwa na rangi ya zambarau. Rangi hii inaanzia pembeni mwa majani na kwenye mashina na baadaye husambaa kwenye jani lote. Rangi inaonekana vizuri zaidi upande wa chini wa jani. Majani ya mwanzo hukauka mapema na mizizi haikui vizuri kwenye mimea yenye upungufu kuliko ile yenye fosfati ya kutosha.

 

3. Upungufu Wa Potashi (Potassium)
Kupungua kasi ya ukuaji wa mimea, ambayo inasababisha mmea kudumaa.
Upungufu ukiwa mkubwa rangi ya kijani inafifia na mwisho kutoweka kabisa na sehemu iliyoathirika inakauka (necrosis) kwenye mazao mengi kama mahindi, mazao mengine ya nafaka na miti ya matunda. Kutoweka kwa rangi ya kijani na kukauka kunaanzia pembeni mwa majani na kwenye ncha. Majani yanakuwa na michirizi ya manjano na vinundu nundu kama migongo ya bati (yellowish streaks and corrugated). Majani ya mwanzo hukauka mapema kwenye mimea yenye upungufu kuliko ile yenye potashi ya kutosha.





Manufaa ya matumizi ya mbolea
i). Kuongeza mavuno
ii). Ubora wa mazao
iii). Kuhifadhi rutuba ya udongo
iv). Kuongeza kipato kutokana na mavuno mengi na bora

Mambo muhimu ya kuzingatia
Ni muhimu kutumia mbolea za viwandani katika kilimo cha mahindi ili kumuwezesha mkulima kupata mavuno mengi. Lakini ikumbukwe kwamba matumizi ya mbolea ni lazima yaambatane na matumizi ya mbinu nyingine bora za kuzalisha mahindi, kama vile:
·      Kuandaa shamba
·      Matumizi ya mbegu bora
·      Kupalilia
·      Kupiga madawa ya kuzuia na kuua wadudu na magonjwa
·      Kuvuna kwa wakati unaostahili
·      Kuhifadhi vizuri mahindi


kwa kumalizia:
Mahitaji ya udongo na mbolea ni muhimu kwa ajili ya ukuaji wa mmea wowote ule, hata hivo mahitaji hayo hutofautiana kati ya mmea moja na lingine kutokana na kutofautiana kwa sehemu ya zao (product) katika hiyo mimea (yaani economic part of a plant). Kwa mfano: mahindi, mpunga sehemu ya zao ni mbegu/punje, wakati nyanya, na bilinganya zao lake ni tunda nakadhalika viazi zao lake ni mizizi!
Hivyo basi ni muhimu ujue zao unalotaka kulima linahitaji nini katika udongo na mbolea ili ufanye maamuzi sashihi.

Acha comment yako hapa chini kwa mchango wowote ule. Pia waweza kuwasiliana nasi

Labels: ,