Kilimo cha Pilipili Mtama


Kilimo-cha-pilipili-mtama
Pilipili mtama au kwa jina lingine pilipili manga ni kiungo muhimu sana katika mapishi. Radha yake ya muwasho ndio kitu hasa kinachotafutwa katika vipunje vidogo vidogo vya zao hili. Pilipili manga husagwa ili kupata ungaunga kabla ya kutumika ingawa pia inaweza kutumika bila kusagwa.


UTANGULIZI

Jina la kitalaam ni Piper nigram na kwa kiingereza ni black pepper. Zao hili asili yake ni Mashariki ya Mbali, na linalimwa zaidi katika mkoa wa Tanga na Zanzibar. Ingawa pia inaweza kukubali katika maeneo ya Kagera

Pilipili nyeusi na nyeupe zote hutumika kwa mapishi ya nyama, samaki na kwa mapishi mengine mbalimbali. Nchi za magharibi zina matumizi makubwa ya viungo hivi. Aidha pilipili mtama nyeusi ndiyo huzalishwa zaidi hapa nchini.


UZALISHAJI

Hali ya hewa na udongo

Viungo vingi humea katika maeneo yenye joto la wastani kati ya nyuzi joto 24-26 na huzalishwa maeneo ya mwambao. Udongo wenye rutuba na unaopitisha maji na wenye uchachu wa kiasi cha pH 6.5. Mahitaji ya mvua ni mililita 1500-2000 kwa mwaka.

Uchaguzi wa mbegu

Uchaguzi huzingatia mambo yafuatayo:-
a) Urefu wa pingili na ukubwa wa majani
b) Ufupi wa pingili unaoambatana na majani madogo.

Tofauti iko hadi kwenye umbile la matunda. Majani ya mche mama sehemu kinapokatwa kipando huondolewa wiki mbili kabla ya kukata. Vipando vyenye macho (nodes) 3-4 humika. Macho mawili huzikwa kwenye udongo na kipando kiwekewe kivuli. Inashauriwa kuweka mbolea ya samadi wakati wa kupanda.


Aina-za-pilipili-manga
Aina za pilipili mtama

Nafasi ya upandaji

Nafasi ya kupanda ni mita 2-3 kati ya mmea na mmea endapo miche imepandwa na miti inayotakiwa kupogolewa mara kwa mara.

Mahitaji ya mbolea

Matumizi ya mbolea hapa Tanzania si makubwa katika kilimo cha viungo. Ingawa kiasi cha kilo 0.4 cha Urea, kilo 0.3 cha Superphosphate na kilo 0.3 cha Potash ya Muriate kinaweza kutumika kwa miche mikubwa.

Miti ya kusimikia miche

Miche hupandwa kwa kusimikiwa nguzo ili ikue kwa kujizungusha kwenye miti kama mijenga ua, n.k. Mti huo wa kusimikia nao pia hupaswa kupunguziwa majani ili kupunguza giza. Kila kabla ya msimu miti hiyo hupaswa kupunguziwa matawi (pruning).

Kupogolea miche ya pilipili mtama

Mche ukifikia miezi 18 inapaswa kupogolea kwa kukata sehemu ya juu ya mche ili kufanya matawi mengine yachipue chini ya mche. Inashauriwa mche kuwa na urefu wa mita 3-3.5.


MASHAMBULIZI YA WADUDU NA MAGONJWA

Hapa nchini hakuna matatizo makubwa ya wadudu na magonjwa.


UVUNAJI NA UHIFADHI NA MASOKO

Uvunaji

Maua ya kwanza hutoka baada ya miaka miwili. Matunda hukomaa miezi tisa (9) hadi kumi (10). Uvunaji ni mizunguko 5 hadi 6 kwa mwaka. Pilipili mtama inaweza kuvunwa kwa misimu miwili. Mavuno ni kati ya tani 0.35 - 3.75 kwa hekta. Wakati wa uvunaji kishina cha matunda ya kijani hukatwa kutoka kwenye mti kisha mbegu za huchambuliwa kutoka kwenye vishina na kisha huanikwa juani kwa siku 3 hadi 4 ili kuhakikisha zinakauka vizuri kabisa. Kiasi cha unyevu kiwe angalau 13 – 14%.


Pilipili-mtama-zilizovunwa



Kuhifadhi

Pilipili mtama iliyokaushwa vizuri inaweza ikawekwa kwenye chombo kisichopitisha hewa na kudumu kwa miaka hadi 20 bila kuharibika. 

Masoko

Soko la pilipili matama linapatikana ndani ya nchi na nje pia. Bei ya ndani ni kati ya Sh1,000-1,500. Zao hili huuzwa katika nchi za Uganda, Kenya, Uingereza, Ujerumani, Mashariki ya Kati, n.k. Bei ya Nje ni wastani wa dola za kimarekani 1,985 kwa tani. (Tafadhali fanyia utafiti soko, data hizi ni za siku  nyingi)

Weka comment yako hapa chini.

Labels: ,