Vitunguu - Kilimo na Hifadhi Bora. Part 2



3.0 KUVUNA NA HIFADHI YA VITUNGUU
Kabla ya kuvuna vitunguu kagua shamba ili kuhakikisha kuwa vitunguu vimekomaa.

Dalili ya vitunguu kukomaa ni:-
· Majani kunyauka na kuanza kukauka
· Asilimia 75 -100% kuangusha shingo na majani kukauka.

Soma KILIMO CHA VITUNGUU Part 1

3.1 KUVUNA
Viitunguu huweza kuvunwa siku 90 mpaka 150 tangu kupanda mbegu kutegemeana na aina. Vitunguu vinavunwa kwa mikono. Mimea inang’olewa au kuchimbuliwa kwa kutumia rato (jembe uma). Baada ya kuvuna vitunguu vinaweza kuachwa shambani vikiwa vimefunikwa na majani kukinga jua kali kwa muda wa siku mbili au tatu kutegemeana na hali ya hewa. Lengo ni kuimarisha ngozi ya vitunguu na kufanya michubuko na majeraha madogo madogo yanayotokea wakati wa kuvuna kuwa magumu na kutengeneza mokovu ambayo yanazuia vimelea vya magonjwa kuingia ndani. Pia kupunguza unyevu kwenye majani na mashina na kuruhusu sehemu ya chini ya shingo kufunga. Ikiwa usalama ni mdogo, vitunguu vinachambuliwa na kukatwa majani na mizizi na kuanikwa sehemu nyingine.
Vitunguu vilivyong'olewa
3.2 KUCHAMBUA
· Tenga vitunguu vilivyooza, kuchubuka na kupasuka. Vitunguu vizuri vikaushwe peke yake.
· Iwapo vitunguu vitahifadhiwa kwa kuninginiza kwenye chaga, basi shingo zisikatwe, bali zisukwe na kufungwa pamoja, na kuninginizwa.
Watu wakichambua vitunguu
3.3 KUKAUSHA
Hatua hii ni muhimu ili kupunguza unyevu, kufanya vitunguu viwe vigumu na kuwa katika hali ya kulala bwete.Vitunguu vinaweza kukaushwa kwa kuninginiza kwenye chaga zilizopangwa mfano wa dari ndani ya banda au kutandaza kwenye kichanja chenye kuruhusu mzunguko wa hewa pande zote, chini ya kivuli sehemu kavu. Epuka kukausha vitunguu chini kwenye aridhini na hasa sehemu zenye jua kali. Jua linababusha vitunguu na kusababisha uharibifu. Ukaushaji huchukua muda wa siku 7 au zaidi kutegemeana na hali ya hewa.

3.4 KUPANGA MADARAJA
Vitunguu vinachambuliwa tena baada ya kukausha ili kuondoa vitunguu vyote vyenye ugonjwa au dalili za ugonjwa, vilivyoota na kutoa mizizi na vyenye shingo nene. Vitunguu vinapangwa kwenye madaraja mbalimbali kufuata ukubwa, umbo au rangi. Hii inawezesha kuapta soko zuri na kuepukana na upotevu mkubwa wakati wa kuhifadhi.

3.5 KUFUNGASHA NA KUWEKA VITAMBULISHO
Mfano wa kifungashio
Vifungashio vinavyopatikana ni mifuko ya nyavu vyenye uwezo wa ujazo wa kilo 20 au magunia ya katani. Mifuko ya nyavu ina ujazo mdogo na pia inarahisisha ubebaji. Magunia ya katani yanatumika lakini yanaficha vitunguu visionekane pia vinachukua mzigo mzito na kuleta usumbufu wakati wa kupakia na kupakua. Vitambulisho vinawekwa kwenye vifungashio ili kusaidia wasafirishaji kujua mzigo ulikotoka na pia kutangaza bidhaa inayohusika kwenye masoko ya nje na ndani.

Kwa soko la nje vitambulisho vinatakiwa na habari zifuatazo:
Mfano wa lebo kwenye paketi ya vitunguu
· Jina la bidhaa mf. Vitunguu Mango’la Red
· Uzito kamili mf. 20 kg
· Jina na anwani ya mkulima au kikundi, jina na anwani ya msafirishaji
· Jina la kijiji wilaya, Mkoa na nchi mf. Igurusi, Mbarali, Mbeya, Tanzania
· Grade 1

Kwa soko la ndani vitambulisho vinakuwa na habari zifuatazo:
· Jina la bidhaa.mf.vitunguu Mango,la Red
· Uzito kamili mf. 20 kg
· Jina la mkulima au kikundi na anwani John Geda au Jitegemee, Box 200, Mbarali Mbeya
· Jina na anwani ya msambazaji mf: Mr. Saidi Mbaga Box 670, Mbeya
Vitunguu vilivyowekwa kwenye magunia
3.6 KUSAFIRISHAJI
Uangalifu wakati wa kupakia, kusafirisha na kupakua ni muhimu ili kuepukana na uharibifu na upotevu wa vitunguu. Mara nyingi vitunguu vinaharibika kutokana na ujazo kupita kiasi kwenye vifungashio na vyombo vya usafiri, pia kutokana na upakiaji na mpangilio mbaya, ambao unasababisha ugandamizaji na kubonyea kwa vitunguu.
Vitunguu vikisafirishwa
Wakati wa usafirishaji yafuatayo yazingatiwe:-
· Kutumia vyombo vya usafiri vinavyofaa hasa magari yenye nafasi ya kutosha na yenye kupitisha hewa
· Kupanga mifuko katika tabaka zenye safu zisizodi tatu
· Mifuko isitupwe wakati wa kupakia na kupakua
· Vitunguu visichanganywe na mazao mengine.

3.7 KUHIFADHI
Vitunguu vinahifadhiwa kwenye maghala bora kama kribu au mabanda ambayo yanaruhusu hewa na paa kuezekwa kwa manyasi ili kupunguza joto.

Vitunguu kwenye kribu
Hifadhi kwenye kribu
Kribu inajengwa kwa fito au mianzi na kuinuliwa juu mita moja toka usawa wa aridhi. Upana wa kribu uwe kati ya sm 60 na 150 ili kuruhusu upepo kupita kwa urahisi. Upepo unaondoa unyevu na joto kwenye vitunguu. Kribu igawanywe sehemu mbili zenye kina cha sm 60 kila moja na kutenganishwa na uwazi was m 30, ili kuruhusu mzunguko wa hewa. 

Wakati wa kutengeneza kribu yaafutayo yazingatiwe:-
· Kribu ijengwe kwenye sehemu yenye upepo
· Kribu iezekwe kwa nyasi ili kudhibiti joto na jua
· Miguu ya kribi iwekwe vizuizi vya panya.
· Weka vutunguu tabaka mbili na kina cha vitunguu kisizidi sm 60

Hifadhi kwa kuninginiza vitunguu kwenye banda
Hili ni banda lenye uwazi mkubwa, lenye upana usiozidi mita tano, na urefu toka chini hadi juu usizidi mita 2½. Banda linajengwa kwa miti, fito, mbao au mianzi na vitunguu vinahifadhiwa kwa kuninginiza kwenye fremu za fito ndani ya banda. Safu za vitunguu hupangwa kufuata urefu wa banda na kimo cha banda. Urefu wa banda huelekezw a kwenye mkondo wa upepo ili kuruhusu upepo kuingia na kutoka. Banda liezekwe kwa nyasi ili kudhibiti joto na jua. Kribu au banda vinahifadhi vitunguu vizuri kwa muda wa miezi sita bila kuharibika.
vitunguu vilivyoning'inizwa
3. 8. UPOTEVU WA VITUNGUU GHALANI
Vitunguu vingi hupotea wakati wa kuhifadhi kwa sababu ya:-
· Kuoza
· Kuota (toa majani na mizizi)
· Kupoteza uzito

3.8.1. KUOZA
Kuoza kwa vitunguu vikiwa ghalani kunasababishwa na vimeliea vya fangasi au bacteia. Joto pamoja na unyevunyevu ndani ya ghala, kunasababisha kuzaliana na kuongezeka kwa vimelea vya magonjwa

Kudhibiti:
· Weka ghala katika hali ya usafi, kausha vizuri na chambua vitunguu ili kabla ya kuhifadhi.

Soma MAGONJWA NA WADUDU WAHARIBFU WA VITUNGUU

a) Muozo Kitako (Bottom rot or basal rot)
Vimelea vya aina ya fungus vinavyoishi kwenye udongo, vinashambulia sehemu ya chini ya vitunguu. Vimelea vinapenya kwenye sehemu zenye michubuko, inayotokea wakati wa palizi, kuvuna au kusafirishwa. Vitunguu vinaoza na baadaye vinakauka na kusinyaa.

Njia zifuatazo zinadhibiti:-
· Mzunguko wa mazao
· Kuchambuaji mzuri kabla ya kuhifadhi
· Kuepuka michubuko wakati wa palizi na kuvuna

b) Ukungu mweusi (Black mould)
Ugonjwa huu unaletwa na vimelea vya fangasi, vinavyoishi kwenye udongo. Vimelea vinazaliana katikati ya maganda na ukungu mweusi kama poda unaonekana. Baadaye maganda yanasinyaa na kuvunjika.

Kudhibiti
· Kutumia mzunguko wa mazao
· Kukagua ghala mara kwa mara na kuondoa vitunguu vilivyooza
· Kuweka ghala katika hali ya usafi.
· Kuondoa masalia ya vitunguu na kuchoma moto.

c) Kuoza shingo (Neck rot)
Vimelea vya fangasi vinashambulia vitunguu vikiwa shambani kabla ya kuvuna. Ugonjwa hauonekani mpaka vitunguu vikomae, vivunwe, vikaushwe na kuhifadhiwa ghalani, ndipo ugonjwa hujitokeza. Ugonjwa unasababisha kuoza kwa vitunguu. Maganda ya vitunguu yanalainika kuanzia shingoni na nyama ya kitunguu huwa na sura ya maji maji. Vitunguu vilivyooza vinyauka na kusinyaa.

Kudhibiti;
· Kukausha vitunguu vizuri kabla ya kuhifadhi
· Kuchoma na kuharibu masalia ya vitunguu shambani na ghalani.

d) Muozo laini (Bacterial soft rot)
Ugonjwa unasababishwa na vimelea vya bacteria. Dalili kubwa ya ugonjwa huu ni kulainika kwa vitunguu na kutoa harufu mbaya. Ukiminya kitunguu maji yenye harufu mbaya yanatoka kwenye shingo. Muozo laini unatokea wakati hali ya hewa ikiwa na unyevunyevu na jotoi. Pia vitunguu vyenye shingo nene ambavyo havijakauka vizuri ni sehemu nzuri sana ya vimelea kuzaliana.

Kudhibiti:
· Ukaushaji wa haraka na wa uhakika baada ya kuvuna unapunguza sana ugonjwa huu

3.8.2 Kuota na kupoteza uzito wa vitunguu
Vitunguu vinakuwa katika hali ya kulala bwete bila kuota kwa zaidi ya miezi sita ikiwa hali ya hewa ghalani ni nzuri. Unyevunyevu mwingi ghalani ni adui mkubwa wa vitunguu vilivyohifadhiwa kwani inasababisha kuota kwa majani na mizizi. Pia hewa ikiwa kavu sana vitunguu hupoteza maji upesi na kusinyaa. Kuongezaka kwa joto na unyevunyevu ndani ya ghala kutokana na mzunguko mbaya wa hewa, uchafu ghalani, ukaushaji na uchambuaji mbaya vinasababisha uharibifu kubwa wa vitunguu ghalani

Kudhibiti ;
· Ghala liwe safi pia liwe na uwezo wa kupitisha hewa kavu na ubaridi wa kutosha.
· Ghala lijengwe sehemu yenye upepo na kuruhusu mzunguko mzuri wa hewa.
· Vifungashio vya vitunguu vipangwe vizuri ili kuruhusu hewa kupita juu na chini.
· Vitunguu ndani ya kribu/ghala vijazwe kina cha sentimeta 30-50.
· Vitunguu vichambuliwe vizuri kabla ya kuhifadhi.
· Vitunguu ghalani vikaguliwe mara kwa mara ili kuondoa vitunguu vilivyoharibika

4.0 SOKO LA VITUNGUU
Kutokana na uhitaji wa matumizi ya kila siku ya zao hili la vitunguu, uhitaji wake umekuwa mkubwa siku kwa siku. Wapo watu walioweza ona fursa hii na kuamua kuifanyia kazi. Kutokana na uhitaji wake kuwa mkubwa inchini kwetu,ni vyema tukaweza jua bei yake ili kumwezesha mtu kutambua uhalisia wake.
Bei ya kuuzia vitunguu shambani wakati was msimu wa vitunguu na endapo vimelimwa kwa wingi basi bei ya gunia inakuwa kati ya shilingi za kitanzania 60,000/= mpaka 80000/=. Inapokuwa sio wakati wa msimu na walimaji wamekuwa wachache na sokoni uhitaji unakuwa ni mkubwa basi bei yake ni kati ya shilling za kitanzania 150,000/= mpaka 200,000/=.  Bei za sadolini kwa sehemu zilizombali na soko ni kati ya shilingi za kitanzania 7,500/= mpaka 8,000/=. Bei ya kilo moja kwa sehemu zilizombali na soko ni kati ya shilingi 2800/= mpaka 3500/=, (hata hivyo bei zinabadlika kulingangana sehemu husika).
Vitunguu vinavyooza

4.1 UUZAJI WA VITUNGUU
Watu wa aina mabalimabali wanahusika na ununuzi na uuzaji wa vitunguu wakiwa ni pamoja na: wakulima, wachuuzi, wafanya biashara ndogondogo, wauza jumla, wauza rejareja, wasafirishaji na madalali.

Ili koboresha uuzaji na kipato ni muhimu kuzingatia yafuatayo:
· Kuboresha ujazo kwa kufuata vipimo vinavyokubalika (kufuta lumbesa)
· Kupeana habari za masoko na bei.
· Kuboresha usafirishaji kwa kutumia vikundi.
· Kuwepo na mtiririko wa kuuza vitungu mwaka mzima, kwa kuboresha hifadhi ikiwa ni pamoja na maghala.
· Kutathimini na kuzingatia ubora wa vitunguu.
· Kutathimini na kuboresha ufungashaji na usafirishaji

HITIMISHO
Tunatambua ya kwamba zao hili linafaida kuanzia shambani mpaka mtumiaji wa mwisho. Sasa ni vyema kabla ya kuanza kilimo hichi kuhakikisha umetatua maswala yafuatayo:
        i.            Eneo (kununua au kukodi),
      ii.            Maji (kilimo cha umwagiliaji au kutegema mvua),
    iii.            Nguvu kazi kwa ajili ya maandalizi ya shamba
    iv.            Msimamizi (Kujua kama utasimamia wewe mwenyewe au utamwajiri mtu kwa kazi hiyo)
  v.       Gharama(gharama za maandalizi,upandaji,ukuzaji, na utafutaji wa masoko na uuzaji)

Soma KILIMO CHA VITUNGUU Part 1


Soma MAGONJWA NA WADUDU WAHARIBFU WA VITUNGUU

Ninaimani ukizingatia haya itakusaidia kujua uanze na mradi wa ukubwa gani. Pia kwa maelezo haya machache itakusaidia kupata mwanga zaidi juu ya fursa hii na endapo utahitaji kuuanza utajua ni wapi pa kuelekea ili kupata maelezo sahihi ya kiutaalamu. acha comment yako hapa chini ikiwa unachochote cha kusema

Labels: , ,